Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia,
Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu ametembelea ujenzi wa Hospitali mpya ya Rufaa
ya Mikoa ya kusini iliyopo mkoani Mtwara na kuridhishwa na kasi ya ujenzi wa
Hospitali hiyo.
Waziri Ummy ameonekana kuridhidhishwa na ujenzi
wa Hospitali hiyo ambao umefikia asilimia 80 na inagharimu Shilingi Bilioni
15.8 mpaka kukamilika kwake.
"Kukamilika kwa Hospitali hii kutasaidia
kupunguza rufaa kwa wananchi wa mikoa ya kusini kwenda kutafuta huduma za
kibingwa Muhimbili, MOI au JKCI, huduma zote zitakua zinapatikana hapa".
Amesema Waziri Ummy.
Waziri Ummy amesema lengo la Wizara ya Afya ni
kuona huduma zinaanza kutolewa katika Hospitali hiyo kabla ya kuanza kampeni za
uchaguzi mwaka huu kwani ilikua ni ahadi ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli
alipopita mwaka 2015 kuomba kura na Hospitali hiyo ipo kwenye utekelezaji wa
ilani ya Chama cha Mapinduzi.
"Hatutaki watu wa Mtwara na mikoa ya
kusini kwa ujumla muende Dar Es Salaam kwa ajili ya kufuata huduma za CT-Scan,
huduma za madaktari bingwa ikiwemo upasuaji wa mifupa, mishipa ya fahamu,
Madaktari wa watoto na uzazi. Huduma zote hizi zitapatikana hapa mara baada ya
ujenzi wa Hospitali hii kukamilika". Amesema Waziri Ummy.
Waziri Ummy amesema kwa ujumla hali ya sekta ya
Afya mkoani Mtwara ni nzuri ambapo katika kipindi cha miaka mitano Hospitali
mpya za Wilaya tatu zimejengwa ambazo ni Nanguluwe, Nanyamba pamoja na Masasi.
Aidha, vituo vya Afya vinane vimejengwa katika Mkoa huo katika kipindi hicho na
kufanya idadi kufikia vituo 23 kutoka 15 wakati Rais Magufuli anaingia
madarakani.
No comments:
Post a Comment