- Asema wananchi Bado wanaamini serikali ni rufaa ya kesi zote walizoshindwa mahakamani.
- Atoa wito Mahakama kujikita katika kutoa Elimu kwa Umma ili jamii iwe na Uelewa wa maswala ya Kisheria
- Apongeza Maboresho makubwa yanayofanywa, hasa matumizi ya Teknolojia ya Habari
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Amos Makalla leo Februari 2, 2022 ameshiriki kilele cha wiki ya Sheria Mkoa wa Dar es Salaam katika Viwanja vya Mahakama ya Kisutu akiwa Mgeni Maalum.
RC Makalla akiongea na hadhara ya Wataalam wa sheria wakiwemo Waheshimiwa Majaji na Mahakimu kuwa uzoefu unaonyesha kuwa aliyetenda kosa iwe ni kubaka, kuua na kesi nyingine yeyote anapokutwa na mkono wa Sheria hawezi kukubali mara zote husema nimebambikiwa kesi na kuendelea kutoa lawama ameonewa, hivyo Waheshimiwa Majaji na Mahakimu wasikate tamaa kazi yao ni ngumu waendelee KUTENDA HAKI.
Aidha RC Makalla amesema wakati anazunguka katika majimbo kusikiliza kero za wananchi alibaini mambo mengi lakini kwa upande wa uelewa wa wananchi juu ya mamlaka ya muhimili wa Mahakama na Serikali bado ni mdogo.
"Utakuta mwananchi anakuja na mgogoro ambao tayari Mahakama inashughulikia au imetoa hukumu za kisheria, bado yeye atalazimisha Mhe. Mkuu wa Mkoa au Mkuu wa Wilaya atengue huku akiamini Serikali ndio kila kitu" Alisema RC Makalla
Hivyo kutokana na uzoefu huo unaonekana kwa Jamii yetu ni vema sasa muhimili huu muhimu wa Mahakama kuelekeza nguvu kubwa au kujikita katika kutoa Elimu kwa Umma juu ya maswala ya Kisheria.
Sambamba na Hilo RC Makalla amepongeza maboresho makubwa yanayofanywa na Mahakama hasa matumizi ya TEHAMA katika Utekelezaji wa majukumu kila siku kwa kuwa matumizi ya Teknolojia ya Habari yanasaidia kuondoa urasimu, rushwa, gharama, lakini pia ufanisi wa kazi kwa kuwa mashauri huweza kusikilizwa mahali popote mtu alipo.
RC Makalla ameahidi kuendelea kushirikiana na Mahakama katika nyanja mbalimbali kwa kuwa Kazi za Serikali hufanywa kwa kutegemeana
Ifahamike kuwa Maadhimisho ya wiki ya Sheria ni kiashiria cha kuanza kwa shughuli za kisheria kwa mwaka mpya 2022 kwani hutoa nafasi ya kutathimini yale yaliyofanyika mwaka iliopita ili kuwa na ufanisi zaidi wa muhimili huo muhimu wa Mahakama.
No comments:
Post a Comment