WATUMIAJI WA NISHATI YA UMEME NCHINI WAFIKIA ASILIMIA 67.75 - Wor'Out Media

Wor'Out Media is a premier site for selected informative articles from Tanzania, East Africa and the rest of the world. We operate 24 hours a day, 365 days a year with complete context, perspective and precision.

Breaking

Thursday, April 6, 2017

WATUMIAJI WA NISHATI YA UMEME NCHINI WAFIKIA ASILIMIA 67.75


Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amesema kiwango cha matumizi ya nishati ya umeme nchini kimeongezeka na kwamba kwa sasa wanaopata fursa ya kutumia nchi nzima ni asilimia 67.75 ambapo maeneo ya vijijini wanaopata fursa hiyo ni 49.5% wakati mijini ikiwa ni 97%.

Profesa Muhongo ameyasema hayo leo jijini Dar es Salaam, katika uzinduzi wa Jukwaa la Nishati Tanzania, ambalo ni matokeo ya mradi wa Tanzania na Uholanzi wa kujenga uwezo katika masuala ya nishati (TDCEB).

“Bara la Afrika watu wasiopata nishati ni 46%. Kwa mujibu wa tafiti iliyofanyika mwezi Disemba 2016 nchini,  inaonyesha Vijijini wanaopata fursa ya kutumia nishati ya umeme ni 49.5%,, miji yetu yote fursa ya kupata umeme ni 97.3%  na kwamba nchi nzima fursa ya kutumia umeme ni  67.5%, hicho ni kiwango cha kimataifa, mpango wa nishati vijijini na mijini umefanikiwa kwa kiwango kikubwa,” amesema.

Hali kadhalika amesema kuwa, tangu mradi wa matumizi bora ya umeme uanzishwe, serikali imefanikiwa kudhibiti upotevu wa umeme unaozalishwa kutoka 25% mwaka 2010 hadi kufikia 19%.

“Matumizi bora ya umeme ni muhimu wakati tulikuwa tunasafirisha umeme mwaka 2010 tulikuwa tunapoteza umeme 25% sasa hivi kwa ajili ya miradi ya matumizi bora ya umeme na uboreshaji wa nyaya kwa kuweka nyaya zilizo bora na transfoma nzuri sasa hivi upotevu wa umeme ni asilimia 19 kwa hiyo ndio maana hiki ni kitu muhimu sababu mnaweza zalisha umeme mwingi lakini unapotea,” amesema.

Kwa upande wa Jukwaa la Nishati, Profesa Muhongo amesema litasaidia uboreshaji wa sera za nishati pamoja na kuongeza wataalamu kwenye sekta ya nishati hasa madini na gesi asilia.

“Jukwaa la nishati limeanzishwa na vyuo vitatu kikiongozwa na UDSM na DIT na Uholanzi kuna vyuo vitatu na kwamba vitashirikiana kupata wataalamu na waalimu wa vyuo, watu wetu watatumia hili jukwaa kwenda kujielemisha masuala ya nishati, vyuo vitawezeshwa kupata vitendea kazi vya kisasa,pia litasaidia kutufanikishia sera ya nishati sababu hili jukwaa malengo yake ni yaleyale ya maendeleo ya milenia,” amesema na kuongeza.

“Malengo yao ifikapo 2030 watanzania wote na watu wengine wote duniani waweze kutumia nishati kwamba tuwe na umeme mwingi wa uhakika unaotabiriaka.”

Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Florens Luoga amesema jukwaa hilo litasaidia kufanikisha azma ya serikali ya kuifanya Tanzania kuwa nchi ya viwanda kutokana kwamba jukwaa hilo litawezesha upatikanaji wa wataalamu wa nishati hasa ya gesi na mafuta ambayo ni sekta nyeti na muhimu katika ukuaji wa sekta ya viwanda.

Kwa upande wa Balozi wa Uholanzi nchini, Jaap Frederiks amesema “Maendeleo ni kuhusu uwekezaji kwa watu kwa kutoa elimu kupitia taasisi na vyuo, hili suala ni muhimu hasa katika sekta ya gesi hususan kipindi hiki ambacho Tanzania imegundulika kuwa na gesi, na kwamba sekta hii hapo baadae itasaidia kuvutia sekta binafsi kutumia rasilimali ya gesi na kuleta manufaa kwa watanzania kupitia fursa za ajira.”

No comments:

Post a Comment

Sharing Buttons

Pages