Wajasiriamali Wanawake walioko chini ya chama cha wafanyabiashara Wanawake Tanzania TWCC wanaoshiriki maonyesho ya biashara ya 44 yajulikanayo kama Sabasaba wameshindwa kuzuia hisia zao za furaha baada ya kushuhudia maelfu ya watu waliokua wakimiminika kwenye banda lao kwaajili ya kuangalia bidhaa zao na kufanya manunuzi.
Wakiongea kwenye mahojiano maalum yaliyolenga kupata mrejesho juu ya mtazamo wao kuhusu maonyesho hayo kwa nyakati tofauti wajasiriamali hao wamesema kuwa hawakutegemea kuona umati mkubwa wa watu makundi kwa makundi wakiingia kwenye banda lao.
Meneja Masoko wa Kampuni inayojishughulisha na tiba ya macho ya Optical Centre ambayo ni mwana chama wa TWCC Willsson Chamshama amesema kuwa banda lao limeweza kupokea na kuhudumia idadi kubwa ya watu tofauti na walivyotajaria.
“kiukweli tumepata watu wengi sana na wametufanya tumekuwa ‘busy’ muda wote, kwakweli mwakani tunaweza kuongeza nafasi.” Aliongea Willson.
“Mzigo niliokuja nao umekaribia kuisha Allhamdullah Sabasaba hii imekuwa nzuri mno tumepata wateja wengia sana tumeuza sana kweli hili sikulitegemea kabisa” alisikika Mjasiliamali wa Korosho kutoka Mtwara Bi Tatu Matango.
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wafanyabiashara Wanawake Tanzania TWCC Mwajuma Hamza amewashukuru wajasiriamali hao kwa kuitikia mwito wa kushiriki kwenye maonyesho kwa wingi licha ya muda wa maandalizi kuwa mchache.
No comments:
Post a Comment