Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Prof. Sifuni Mchome (kushoto) akizungumza jambo kwenye ofisi za eneo la ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) unaoendelea Jijini Arusha, kushoto ni Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha Mhe. Moses Mzina.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Prof. Sifuni Mchome akiwa katika picha ya pamoja.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Prof. Sifuni Mchome akisaini kitabu cha wageni kwenye ofisi za eneo la ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) unaoendelea Jijini Arusha, kushoto ni Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha Mhe. Moses Mzina.
Na: Catherine Francis – Mahakama, Arusha.
Katibu mkuu Wizara ya Sheria na Katiba, Prof. Sifuni Mchome amepongeza kasi ya maendeleo ya ujenzi wa jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) unaoendelea Jijini Arusha.
Pongezi zimetolewa na Mchome alipotembelea na kufanya ukaguzi wa maendeleo ya ujenzi wa jengo hilo, Julai 9, mwaka huu, ambapo alisema kulingana na muda ambao limeanza kujengwa hadi sasa hatua waliyofikia ni nzuri na inaridhisha.
‘‘Wahandisi wanaohusika na ujenzi huu endeleeni na kasi hiyo na ikiwezekana mmalize mapema zaidi kabla ya mwezi Desemba kama ilivyokubaliwa awali ili kuweza kuruhusu upatikanaji wa huduma za kisheria kwa haraka na mapema zaidi,’’alisema Katibu Mkuu huyo.
Aidha Mchome alipata nafasi ya kutembelea ofisi ya Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Mhe. Moses Mzuna ili kuweza kujadili mafanikio na changamoto za ujenzi huo.
Naye Mtendaji Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Bw.Edward Mbara, aliwasilisha ripoti ya ujenzi huo na kuzitaja changamoto kubwa walizokumbana nazo kuwa hali ya hewa ya mvua pamoja na ucheleweshaji wa malipo kwa wakandarasi kutoka Hazina.
Akitatua changamoto ya uchelewashaji wa malipo hayo, alipiga simu kwa wahusika papohapo jambo ambalo lilipatiwa ufumbuzi na kupewa majibu ya kuridhisha
Katika ziara hiyo Mchome aliambatana na uongozi wa Mahakama Kuu Tanzania Kanda ya Arusha walitembelea ujenzi huo ili kujionea hali halisi.
No comments:
Post a Comment