Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID) na Tanzania Zaungana Kupambana na Usugu Wa Vimelea Vya Magonjwa Dhidi ya Dawa (UVIDA) na Magonjwa Ya Zuonotiki - Wor'Out Media

Wor'Out Media is a premier site for selected informative articles from Tanzania, East Africa and the rest of the world. We operate 24 hours a day, 365 days a year with complete context, perspective and precision.

Breaking

Sunday, May 26, 2024

Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID) na Tanzania Zaungana Kupambana na Usugu Wa Vimelea Vya Magonjwa Dhidi ya Dawa (UVIDA) na Magonjwa Ya Zuonotiki

Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Godwin Mollel (kushoto) na Kaimu Mkurugenzi wa Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID), Alex Klaits, wakizindua kampeni ya “Holela-Holela Itakukosti” inayolenga kueleimisha jamii juu ya udhibiti wa usugu wa vimelea vya magonjwa dhidi ya dawa (UVIDA) na magonjwa ya kipaumbele ya zoonotiki (magonjwa yanayoambukizwa kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu). Kampeni hii inaratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Wizara ya Afya, Wizara ya Mazingira, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, na Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID).
Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Godwin Mollel, akihutubia washiriki wakati wa uzinduzi wa kampeni ya “Holela-Holela Itakukosti” inayolenga kueleimisha jamii juu ya udhibiti wa usugu wa vimelea vya magonjwa dhidi ya dawa (UVIDA) na magonjwa ya kipaumbele ya zoonotiki (magonjwa yanayoambukizwa kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu). Kampeni hii inaratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Wizara ya Afya, Wizara ya Mazingira, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, na Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID).

Dar es Salaam, Tanzania – Jumapili Mei 26, 2024 | Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Wizara ya Afya, Wizara ya Mifugo na Uvuvi na Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID), wanajivunia kuzindua kampeni ya "Holela-Holela Itakukosti" ambayo imezinduliwa Jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki. Kampeni hii unasisitiza mbinu kamilifu ya "Afya Moja" kushughulikia tatizo la UVIDA na magonjwa ya zuonotiki.

Kampeni ya "Holela-Holela Itakukosti," ambayo inamaana ya "uzembe unagharimu," inaonyesha uhusiano muhimu kati ya afya ya binadamu, afya ya wanyama, na mazingira. Kwa kutumia mkakati wa sekta mtambuka, kampeni inalenga kushughulikia sababu mbalimbali za kijamii zinazopelekea tatizo la UVIDA na magonjwa ya zuonotiki.

Kampeini ya Holela Holela inaonyesha athari za UVIDA na magonjwa ya zuonotiki, ikisisitiza umuhimu wa matumizi sahihi ya dawa na kufuata miongozo ya matibabu ili kuzuia kuenea kwa maambukizi sugu. Vile vile, Wizara ya Afya, Wizara ya Mifugo na Uvuvi zina jukumu muhimu katika kampeni, zikitambua kwamba matumizi yasiyo sahihi ya dawa kwa binadamu na wanyama, yanachangia kwa kiasi kikubwa katika kuongezeka kwa tatizo la UVIDA.

Akizungumz Jijini Dar es Salaam wakati wa kuzindua kampeini hiyo, Mkurugenzi wa Usimamizi wa Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Brigedia Generali Hosea Ndagala alisema "Kushughulikia tatizo la UVIDA na magonjwa ya zuonotiki kunahitaji mbinu ya jumla inayojumuisha afya ya binadamu, afya ya wanyama, na afya ya mazingira” huku akiongeza "Mkakati wetu wa – ‘Afya Moja' unahakikisha tunashughulikia masuala haya kwa ujumla wake, tukikuza tabia endelevu katika sekta zote."

Tabia duni za ufugaji, kama vile msongamano wa wanyama na udhibiti duni wa magonjwa, husababisha milipuko ya mara kwa mara ya magonjwa ya kuambukiza kwa wanyama. Hii, kwa upande mwingine, inapelekea wafugaji kutumia dawa mara kwa mara na hivyo kuchangia kuongezeka kwa tatizo la UVIDA” alisema Brigedia Ndagala huku akisisitiza kuwa uharibifu wa mazingira na usimamizi mbaya wa taka huchochea zaidi kuenea kwa vijidudu vinayosababisha magonjwa sugu na vimelea vya vinayosababisha magonjwa ya wanyama, na hivyo kuleta maambukizi yanayoathiri wanyama na binadamu.

Alex Klaits, Kaimu Mkurugenzi wa USAID alisisitiza umuhimu wa juhudi za pamoja, akisema, "Kampeni inaonyesha jukumu muhimu la ushirikiano katika kuleta athari chanya na kuhakikisha uendelevu wa muda mrefu, ikiwaleta pamoja wadau wa Afya moja kutoka sekta mbalimbali kupambana na UVIDA na magonjwa ya zuonotiki".

Mkurugenzi Msaidizi wa Afya Moja, Ofisi ya Waziri Mkuu, Dkt. Salim Manyatta kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi alisisitiza jukumu muhimu la usimamizi mzuri wa mifugo, "Kuboresha mbinu za ufugaji wanyama na kuhakikisha wafugaji wanafuata ushauri wa wataalamu wa mifugo ni mbinu muhimu zaidi dhidi ya UVIDA na magonjwa ya zuonotiki. Juhudi zetu katika kampeni hii zitasaidia kulinda afya ya wanyama na binadamu."

Kampeni itasambaza seti kamili ya nyenzo zitakazotumika na wanahabari, waelimishaji katika ngazi ya jamii, watoa huduma za afya na viongozi wa dini. Nyenzo hizo zina taarifa ya kutosha kuhusu uhusiano kati ya afya ya binadamu, wanyama, na mazingira na kuhamasisha tabia za kujikinga na UVIDA na magonjwa ya zuonotiki.

Kampeni ya "Holela-Holela Itakukosti" inaashiria hatua mbele katika juhudi za Tanzania kupambana na UVIDA na magonjwa ya zuonotiki kupitia mpango wa ‘Afya Moja’. Kwa kuziunganisha sekta za afya ya binadamu, wanyama, na mazingira, kampeni inalenga kuweka mustakabali endelevu kwa watanzania wote.
Kaimu Mkurugenzi wa Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID), Alex Klaits, pamoja na mwakilishi wa shirika hilo, Lulu Msangi, wakiwa kwenye picha ya pamoja na balozi wa kampeni ya "Holela-Holela Itakukosti" inayolenga kueleimisha jamii juu ya udhibiti wa usugu wa vimelea vya magonjwa dhidi ya dawa (UVIDA) na magonjwa ya kipaumbele ya zoonotiki (magonjwa yanayoambukizwa kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu). Kampeni hii inaratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Wizara ya Afya, Wizara ya Mazingira, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, na Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID).

No comments:

Post a Comment

Sharing Buttons

Pages